Home Makala MJADALA WA KIBU HAUNA AFYA KWA SOKA LETU

MJADALA WA KIBU HAUNA AFYA KWA SOKA LETU


 MNAPOKUWA na jambo hasa linalozua 
mjadala, mwisho wake lazima kuwe na faida ambayo itatokana na mlichokuwa mnakijadili. Kama hakuna kitu, hakuna sababu ya kuwa na mjadala.

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kupitia Waziri wa Mambo ya Ndani, George Simbachawene imechukua uamuzi wa kumpa Kibu Denis uraia wa Tanzania.

Uamuzi huo ulitokana na kugundulika uraia wake ulikuwa na walakini, hivyo suala la ufuatiliaji kupitia Idara ya Uhamiaji ambao ndio wataalamu likafanyika na majibu yamepatikana.

Idara ya Uhamiaji Tanzania, ni moja ya idara zinazofanya kazi zake kwa ubora wa juu kabisa. Idara hiyo ina wataalamu wengi wa kutosha ambao wana ujuzi na uzoefu na kazi yao kuhusiana masuala ya kidiplomasia.

Unaweza ukajiuliza, wale ambao wamekuwa wakihoji kwa nguvu kubwa suala la Kibu wana ushahidi upi, wanataka kutuonyesha nini na mwisho wake ni upi au wanataka nini?

Hakuna anayezuiwa kuhoji lakini mjadala utakuwa na faida gani, kwanini watu wanahoji na kwa sababu gani hasa wanataka kufanya hivyo?

Ukiangalia ndani ya mjadala huo unagundua inatumika nguvu nyingi sana kujadili au kuhamasisha mijadala kwa kuwa tu kijana huyo sasa yuko Simba.

Zile siasa za watani zimeshika hatamu na mambo mengi yasiyokuwa na sababu za msingi ndio yamechukua sehemu kubwa.

Kumbuka alicheza moja ya timu ndogo za Wilaya ya Ngara, hakukuwa na mjadala. Akacheza Geita Gold Mine, kimya, akacheza Mbeya City, hatukusikia kitu na hata akacheza timu ya taifa, Taifa Stars bado ilikuwa poa tu.

 Yuko Simba, kelele zimeshika hatamu.Vizuri, labda kelele hizo zilichangia leo wataalamu wa Idara ya Uhamiaji waifanye kazi yao vizuri na mwisho wamekamilisha na kumaliza utata wa suala hilo kwa kufuata utaratibu sahihi.

Leo kijana huyo anaweza kulitumikia taifa la Tanzania na tunaona ni sehemu ya mchango mzuri.Sasa wanaotaka kuendelea kulikuza na kutaka kuionyesha jamii kama hata watalaamu wa Idara ya Uhamiaji hawajui lolote, ni kutaka kujenga na kuupa nguvu uchochezi ambao hauna afya wala faida kwa taifa na mpira wa Tanzania.

SOMA NA HII  NDEMLA UMELIKUNG'UTA VUMBI, SASA NI WAKATI WAKO KUONYESHA UWEZO

Wewe unaipenda Yanga, Kibu akaichezea Simba na Taifa Stars, unapata hasara ipi. Au wewe ni Coastal, huyu sasa kapewa uraia, au suala lake limewekwa sawa, hasara yako ni nini?

Tunaweza kujifunza kwa kujadili mambo mengi ya msingi ambayo mjadala wake unakuwa ni faida kwa taifa leo na kama ni soka basi soka letu badala ya ule ushabiki wa chuki na kelele zisizokuwa na sababu za msingi.

Kama Kibu ana nafasi nzuri ya kutoa mchango mkubwa kwa taifa letu kupitia Simba au timu ya taifa, au siku zijazo kupitia Yanga au timu nyingine, basi bora liwe kwa faida ya mpira wetu.

Hakuna sababu ya kutengeneza drama kuhusiana naye sababu ya hisia za kishabiki za ule ushabiki wa Yanga na Simba ambao kila mmoja kazi yake ni kumuombea mpinzani wake njaa.

Hata mara moja, hilo halijawahi kuwa na faida zaidi ya kutengeneza maneno mengi ya upotezaji muda ambayo pia mara nyingi yamekuwa hayana faida hata kidogo.

Tubadilike, tuthamini muda wetu na kuachana na kupoteza nguvu kwa mambo yasiyo na tija. Pia tukubali,wataalamu wa masuala ya uraia, wako Idara ya Uhamiaji Tanzania, tuiheshimu badala ya kubwabwaja huku tukiwa hatuna hoja ya msingi wala utaalamu wa kile tunachozungumza tu hewani.