Mtendaji Mkuu wa zamani wa Yanga, Senzo Mbatha Mazingiza, amesema anaiona ikitinga nusu fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika msimu huu kutokana na ubora iliouonesha.
Senzo ambaye kwa sasa ni CEO katika Shirikisho la Soka Botswana, anakumbukwa kwa utendaji wake wenye mafanikio ndani ya Yanga na Simba akiwa hapa nchini.
Akizungumza nasi, Senzo alisema kwa kiasi kikubwa ubora ambao wameuonesha katika Kombe la Shirikisho Afrika msimu huu, wana uwezo mkubwa wa kusonga mbele na kutinga hatua inayofuata ya nusu fainali.
“Yanga mpaka sasa wamecheza vizuri sana, ukiwatazama kwa jinsi ambavyo wameingia robo fainali utabaini ni timu ambayo ina nguvu kubwa sana katika michuano hii, ninaamini watafika mbali zaidi ya walipofika sasa.
“Yanga wanaweza kutinga nusu fainali, uwezo huo wanao, hata wapinzani ambao watakutana katika robo fainali wote nikiwaangalia naona kabisa wanayo nafasi ya kufika mbali, natamani kuona ikifika hata fainali ya michuano hii,” alisema kiongozi huyo.