FARID Mussa ndiye alikuwa shujaa akitokea benchi na kuifungia bao la ushindi Yanga dhidi ya TP Mazembe huku akisema ukuta wa wapinzani wao ulikuwa mgumu.
Farid alifunga bao hilo na Yanga kufikisha pointi 13 kwenye kundi D ikifuatiwa na US Monastir nao wakiwa na pointi hizo lakini inashika nafasi ya pili kwa tofauti ya mabao.
Farid alisema; “Nilipokuwa benchi kocha alinisisitiza kuwasoma mabeki wao huku akinisisitiza pia kuwa kwa asilimia kubwa ni wachezaji ambao hawakuwaona mchezo wa kwanza hivyo baada ya kupata nafasi na wao waliingia kuonyesha walichonacho ndio ugumu tuliokutana nao”
“Bao nililofunga lilikuwa linahitaji maamuzi ya haraka kama nilivyofanya kwani ulikuwa ni mpira wa kutemwa na sio makosa ya mabeki nilipoipata hiyo nafasi sikutaka kufanya mambo mengi nilijiweka sawa na kukwamisha mpira nyavuni na nashukuru ndilo lilikuwa bao la ushindi,” alisema.