Home Habari za michezo KUHUSU ISHU YA MKUDE NA NA KYOMBO KWENDA KUKIPIGA ULAYA…UKWELI WOTE HUU...

KUHUSU ISHU YA MKUDE NA NA KYOMBO KWENDA KUKIPIGA ULAYA…UKWELI WOTE HUU HAPA…

Habari za Simba leo

Wakati uongozi wa Simba ukikuna kichwa kwa Banda na Sawadogo, habari kutokana ndani ya kikosi hicho kinasema kuwa, Simba ipo kwenye mipango ya kuwapeleka Ulaya baadhi ya wachezaji wake ambao hawajapata muda wa kutosha kucheza ili wakacheze huko West Armenia inayoshiriki Ligi Daraja la Kwanza nchini Armenia.

Simba imefikia maamuzi hayo baada ya kuingia mkataba wa kimahusiano na timu hiyo siku chache zilizopita na uongozi wa West Armenia upo Tanzania na uliukuwa mubashara katika mechi ya mwisho ya ligi iliyozikutanisha Simba na Coastal Union uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam na kuzungumza na baadhi ya Wachezaji.

Mmoja ya watendaji ndani ya Simba alisema kuwa Habib Kyombo, Jonas Mkude, Mohamed Mussa, Nassor Kapama na Jimmyson Mwanuke ndio majina ambayo viongozi wa Armenia wamepewa ili kuwatazama kama watawafaa na baada ya hapo mazungumzo yataanza.

“Hata mechi ya mwisho tulikuwa nao pale uwanjani, wanataka wachezaji watatu hadi wanne kwa kuanzia na majina hayo niliyokutajia ndio wamepewa, hivyo watachagua wao kisha mazungumzo ya mikataba na mambo mengine yataendelea kwani bado wako Dar na wataondoka baada ya kumaliza kila kitu.” alisema mtu huyo.

Ofisa Mtendaji Mkuu wa Simba, Imani Kajula alisema walisaini mkataba wa kimahusiano na West Armenia ambapo miongoni mwa vitu vilivyopo ndani ya mkataba huo ni kubadilisha wachezaji, ujuzi na kuendeleza soka la vijana.
“Makubaliano baina yetu na wao yana fursa sana kwetu na kwa wachezaji.

Miongoni mwake ni kutoa fursa kwa wachezaji wetu ambao hawapati muda wa kutosha kucheza kwenye timu kubwa kwenda kucheza huko, lakini pia kushirikiana katika kuendeleza soka la vijana,” alisema Kajula

Ikumbukwe Mkude, Kyombo, Mwanuke na Mussa ni miongoni mwa wachezaji wa Simba ambao kocha mkuu wa chama hilo, Roberto Oliveira ‘Robertinho’ hajawaweka kwenye mipango yake ya msimu ujao na amependekeza wasajiliwe mafundi wengine kwenye maeneo yao.

SOMA NA HII  NYOTA WANNE WA SIMBA WAACHWA BONGO, MORRISON NAYE YUPO KWENYE ORODHA