Home Habari za michezo CHAMPIONSHIP MUAMUZI AZUA GUMZO…ISHU IKO HIVI

CHAMPIONSHIP MUAMUZI AZUA GUMZO…ISHU IKO HIVI

Mwamuzi wa kati Selugwani Shija ameleta gumzo kwenye Ligi ya Championship jana katika mchezo kati ya Biashara United ya Maea dhidi ya Mbeya City katika Uwanja wa Nyamagana, Mwanza.

Mchezo huo wa mzunguko wa tisa umechezwa jana Novemba 3, 2023 saa 10:00 jioni. ukiambatana na mvua na Biashara akaibuka na ushindi wa mabao 2-1.

Tukio lilotea gumzo uwanjani ni baada ya Cyprian Kipenye kufunga bao dakika ya 20 kwa mpira wa kutenga uliomshinda kipa, Jeremiah Kisubi ambaye aliudaka lakini mwamuzi wa pembeni akadai ameudakia ndani hivyo kuwapa bao wenyeji.

Uamuzi huo ulizua vuta nikuvute kwa wachezaji na benchi la ufundi la Mbeya City ambao hawakukubaliana na maamuzi hayo ya refa wa mchezo huo, Selugwani Shija na kutishia kutoendelea na mchezo huku kipa wa timu hiyo, Jeremiah Kisubi akigoma kurudi langoni akisisitiza mpira haukuvuka msitari.

Mvutano huo umedumu kwa takribani dakika saba ndipo wachezaji wa Mbeya City wakakubali kuendelea na mchezo ambapo mwamuzi wa akiba Haji Vemba ameongeza dakika tano za kipindi cha kwanza.

Hata hivyo mwamuzi, Selugwani Shija alimaliza mchezo kabla ya dakika hizo kumalizika ndipo benchi la ufundi la Mbeya City likalalamika huku mwamuzi wa akiba akimkumbusha kwa kumuonyesha vidole viwili kuwa bado dakika mbili.

Mwamuzi huyo aliruhusu mchezo kuendelea kumalizia dakika hizo mbili, ambapo dakika 45 za kwanza zimemalizika Biashara United wakiwa mbele kwa bao 1-0.

Kipindi cha pili, wageni wamekuja juu wakilisakama lango la Biashara United, ambapo wamefanikiwa kusawazisha bao hilo dakika ya 60 kupitia kwa Shaban Ada ambaye amemalizia mpira ambao umetemwa na kipa, David Kissu.

Biashara united imepata bao la pili la ushindi dakika ya 80 likifungwa na Thomas Malulu kwa shuti kali ambalo limemshinda kipa, Kisubi hivyo kuihakikishia ushindi timu yake.

Biashara United imetumia Uwanja wa Nyamagana uliopo Mwanza baada ya Uwanja wao wa nyumbani, Karume kufungiwa kwa kutokidhi vigezo, ambapo mchezo wao wa kwanza baada ya adhabu hiyo walitumia Kaitaba uliopo Bukoba

SOMA NA HII  UNAWEZA KUMALIZA JUMAPILI BILA KUKUBASHIRI NA MERIDIAN BET