Home Habari za michezo RASMIII….COASTAL UNION WAIPELEKA CAF TANGA….MTIBWA SUGAR CHALIIII 😵‍💫😵‍💫….

RASMIII….COASTAL UNION WAIPELEKA CAF TANGA….MTIBWA SUGAR CHALIIII 😵‍💫😵‍💫….

NBC Premier League

WAGOSI wa Kaya, Coastal Union wamejihakikisha nafasi ya kushiriki michuano ya kimataifa msimu ujao baada ya leo kukata tiketi ya CAF kwa kutoka suluhu na JKT Tanzania kwenye Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga, kwani sasa imefikisha pointi 42 ambazo haziwezi kufikiwa na KMC iliyokuwa ikiifukuzia iliyo na pointi 36 na hata kama zitashinda mechi za mwisho zitafikisha 39.

KMC ilikuwa na uwezo wa kuzifikia pointi hizo 42, lakini kipigo cha leo kutoka kwa Simba kimeitibulia na kuiacha ibaki katika nafasi ya nne.

Matokeo ya KMC yameirahisishia Coastal kukata tiketi ya kucheza michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika msimu ujao sambamba na vigogo, Simba, Yanga na Azam.

Mara ya mwisho kwa Coastal kushiriki michuano ya kimataifa ilikuwa mwaka 1989 iliposhiriki Kombe la Washindi Afrika na kuishia raundi ya kwanza. Michuano hiyo ilikuja kuunganishwa na Kombe la CAF na kuzaliwa kwa Kombe la Shirikisho Afrika mwaka 2004.

Coastal inakuwa timu ya sita kukata tiketi ya CAF ikiwa nafasi ya nne baada ya KMC, Namungo, Biashara United, Geita Gold na Singida Fountain Gate, kutokana na Tanzania kupewa nafasi ya timu nne katika michuano hiyo, mbili zikicheza Ligi ya Mabingwa na nyingine Kombe la Shirikisho.

Yanga ndio bingwa wa Ligi Kuu na ipo fainali ya Kombe la Shirikisho (FA) linalotoa mwakilishi wa Kombe la Shirikisho Afrika sambamba na Azam iliyopo nafasi ya pili katika Ligi Kuu, huku Simba ikiwa ya tatu na Coastal ikiwa ya nne.

Kama Yanga ingeingia fainali ya CAF na timu nyingine nje ya hizo mbili zilizopo nyuma yake na timu hiyo kubeba, Wagosi wasingekuwa na nafasi, kwani bingwa wa Ligi na mshindi wa pili wangekata tiketi ya Ligi ya Mabingwa na bingwa wa FA na mshindi wa tatu wa Ligi Kuu wangeenda Kombe la Shirikisho Afrika.

MTIBWA NDIO BASI TENA…

MABINGWA wa zamani wa Tanzania msimu wa 1999 na 2000, Mtibwa Sugar imeshuka rasmi jana baada ya kufumuliwa mabao 3-2 na Mashujaa katika mechi iliyopigwa kwenye Uwanja wa Lake Tanganyika mjini Kigoma.

Mtibwa iliyoanzishwa mwaka 1988 na kupanda Ligi Daraja la Kwanza (sasa Ligi Kuu) 1996, imeshuka kutokana na kusaliwa na pointi 21 ikiwa na mechi moja mkononi ambayo hata ikishinda haiwezi kuiokoa kwani tayari pointi hizo zimeshapitwa na timu nyingine zilizopo juu yake.

Kanuni za Ligi Kuu ni kwamba, timu zinazoshika nafasi mbili za mwisho zinashuka moja kwa moja na zile zinazomaliza nafasi ya 13 na 14 zinacheza mchujo (play-off) zenyewe kwa zenyewe na mshindi husalia katika ligi hiyo na ile inayopoteza inacheza na mshindi wa mechi kama hizo kwa timu za Ligi ya Championship.

Mabao yaliyoizamisha Mtibwa iliyokwenda Kigoma bila Kocha Mkuu, Zubeiry Katwila na yule wa makipa, Patrick Mwangata pamoja na meneja wa timu Henry Joseph na kuachiwa kocha msaidizi, Awadh Juma, yaliwekwa kambani na Reliant Lusajo aliyefunga mawili dakika ya tatu na 26 na lile la Mundhir Vuai la dakika ya 32.

Mtibwa ilipata mabao ya kufutia machozi kupitia kwa Rashid Seif Karihe aliyefunga katika dakika ya 15 na Samson Madekele alijifunga katika harakati za kuokoa dakika ya 55.

Ushindi huo umetoa nafuu kwa Mashujaa kwani imefikisha pointi 32 ikiwa nafasi ya 11 na sasa inasikilizia mchezo wa mwisho dhidi ya Dodoma Jiji ukitarajiwa kupigwa Jumanne kwenye uwanja wa nyumbani, Kigoma na iwapo itaibuka na ushindi itasalimika hata kucheza play-off.

Mtibwa sasa inasubiri kukamilisha ratiba Jumanne ugenini kucheza na Ihefu ambayo leo imeicharazwa mabao 2-0 na Dodoma Jiji katika pambano lililopigwa Uwanja wa Liti, mjini Singida.

TZ PRISONS UHAKIKA AISEEE..

MAAFANDE wa Tanzania Prisons imejihakikisha kusalia katika Ligi Kuu Bara baada ya leo kupata sare ya 2-2 ikiwa ugenini mbele ya Namungo na kutuliza presha za mashabiki ambao mwanzoni mwa msimu waliishi kwa mawazo kutokana na timu kufanya vibaya.

Matokeo hayo yameifanya Prisons kufikisha pointi 34 na kusalia nafasi ya tano nyuma ya KMC, hivyo kuwa miongoni mwa timu zenye uhakika wa kushiriki ligi ijayo, kwani alama ilizonazo zimeziweka salama.

Mabao yaliwekwa kimiani na Khamis Zabona dakika ya 33 na Benedicto 61 yaliiweka Prisons katika nafasi nzuri ya kurejea Nne Boram, lakini wenyeji walipindua meza kwa kuchomoa moja baada ya jingine kupitia kwa Mrundi Derick Mukombozi aliyefunga dakika ya 58 na 84.

Prisons itajilaumu kwa kushinda kutoka na ushindi mjini Lindi, kwani iliongoza kwa muda mrefu na kupanda nafasi ya nne ikiing’oa KMC, kabla ya bao la Mukombozi kuitibulia na kuifanya iambulie sare hiyo na pointi moja.

Katika mechi nyingine iliyopigwa mjini Singida, wenyeji Ihefu ilikubali kipigo cha mabao 2-0 kutoka kwa Dodoma Jiji katika pambano la Dabi ya Kanda ya Kati.

Mabao ya washindi yalifungwa na Yassin Mgaza dakika ya saba na Mghana Christian Zigah aliyetupia dakika moja kabnla ya filimbi ya mwisho na kuifanya Dodoma kufikisha pointi 33 ikilingana na Namungo, Singida na Ihefu.

GEITA GOLD UWIIII….

WACHIMBA Dhahabu wa Geita, Geita Gold, wameendelea kujiweka pabaya katika Ligi Kuu Bara baada ya leo kufumuliwa mabao 2-1 na Singida Fountain Gate kwenye Uwanja wa Nyamagana jijini Mwanza na sasa watalazimika kushinda mechi ya Jumanne mbele ya Azam iwapo hawataki kushuka daraja moja kwa moja.

Geita ipo nafasi ya pili kutoka mkiani ikiwa na pointi 25 na kama itashinda itafikisha 31 na kusikilizia matokeo ya timu hiyo kuona itacheza play-off au itaungana na Mtibwa Sugar kwenda Ligi ya Championship baada ya mabingwa hao wa zamani kushushwa rasmi leo na Mashujaa.

Katika mechi hiyo, Singida inayopambana nayo kujiokoa na janga la kushuka daraja au kucheza play-off ilianza mapema kupata mabao kupitia kwa Nicholas Gyan aliyefunga dakika ya saba ya mchezo kabla ya Amos Kadikilo kuongeza jingine akimalizia pasi ya Deus Kaseke.

Geita ilipata bao la kufutia machozi katika dakika ya 54 na Erick Kyaruzi akimalizia pasi ya Anthony Mlingo.

Ushindi huo umeifanya Singida kufikisha pointi 33 ikishika nafasi ya saba na sasa inajiandaa kuikaribisha Kagera Sugar ambayo leo imefumuliwa mabao 4-1 na Azam jijini Dar es Salaam.

Credit:- MwanaSpoti

SOMA NA HII  A-Z JINSI SIMBA ILIVYOIFINYANGA RUVU SHOOTING JANA...BOCCO ATOA GUNDU LA MIEZI TISA...