Home Habari za michezo AHMED ALLY:- KOMBE LA SHIRIKISHO TUKIENDA VIBAYA TUNAKULA ZA USO MAPEMA TU…

AHMED ALLY:- KOMBE LA SHIRIKISHO TUKIENDA VIBAYA TUNAKULA ZA USO MAPEMA TU…

Habari za Simba leo

Meneja Habari na Mawasiliano wa Klabu ya Simba, Ahmed Ally amewataka mashabiki na Wanachama wa Klabu hiyo kuacha kuidharau michuano ya Kombe la Shirikisho Barani Afrika ambayo wamekuwa wakiitaja kama michuano ya walioshindwa ‘losers’ wakidai kwamba ni kombe dogo ambalo halina hadhi.

Ahmed amesema hayo siku chache baada ya Ligi Kuu kutamatika huku Simba wakimaliza nafasi ya tatu katika msimamo wa ligi hiyo ambapo wameangukia kwenye michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika ambayo watashiriki msimu ujao jambo ambalo amesema hayakuwa malengo yao kabisa.

“Tumeangukia Kombe la Shirikisho ambapo hakuna Mwanasimba anayefurahi kwenda kushirki Kombe la Shirikisho, lakini hatuna budi kuliheshimu kombe hilo na kuwekeza nguvu zaidi ya kwenda kufanya vizuri katika michuano hiyo.

“Kila Mwanasimba alitamani kuiona timu yake ikishiriki Ligi ya Mabingwa Afrika kwa sababu ni mashindano makubwa na ndiyo hadhi yetu na ni fahari yetu pia kushiriki michuano hiyo, lakini bahati mbaya imekuwa kinyume chake na tumeenda kushiriki kombe la shirikisho.

“Kwanza kila Mwanasimba anatakiwa kuheshimu shindano hilo ili kuheshimu nafasi ya kufanya vizuri shindano hilo. Tusiseme tu ni Kombe la Shirikisho halafu tukaishia hapo, lazima tujiandae, sio kombe la kawaida kawaida, wapo wakubwa wa kombe hilo kama Berkane, Pyramids, USM Alger ambao ukienda kichwa kichwa unaweza kuishia pabaya.

“Niwaombe Wanasimba hata kama tunalichukia Kombe la Shirikisho hatuna budi kuliheshimu na kufanya maandalizi makubwa ili twende tukafanye vizuri kwenye kombe hilo. Aibu itakuja pale unakwenda Kombe la Shirikisho nalo unashindwa kufanya vizuri.

“Ukienda Shirikisho ukafanya vizuri unatoa ujumbe kuwa mimi hadhi yangu ni Ligi ya Mabingwa lakini kwa bahati mbaya nimekuja Kombe la Shirikisho.Tuache stori za kipuuzi na za wapuuzi kwamba ni kombe dogo, ni kombe ambalo tunapaswa kuingia kwa heshima kubwa, tukicheza vijana watatudhalilisha ukweni,” amesema Ahmed.

SOMA NA HII  YANGA YA MSIMU HUU NI HATARI CHEKI ILICHOFANYA KWENYE MECHI ZA KUJIPIMA LEO