Home Uncategorized KELVIN YONDANI ATAJWA ZESCO UNITED

KELVIN YONDANI ATAJWA ZESCO UNITED


Beki kisiki wa Yanga, Kelvin Yondani, anaonekana kuwa tishio mbele ya kikosi cha Zesco United baada ya kocha mkuu wa kikosi hicho, Mzambia, George Lwandamina, kuweka wazi kuwa, beki huyo ni miongoni mwa mabeki bora ambao amewahi kuwafundisha.

Kauli ya Lwandamina imekuja zikiwa zimebaki siku chache kabla ya Yanga haijavaana na Zesco United katika mchezo wa hatua ya kwanza ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

Yanga na Zesco United zitaumana Septemba 14, mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam katika mchezo wa raundi ya kwanza wa michuano hiyo, kabla ya kurudiana Septemba 27, mwaka huu nchini Zambia.

Lwandamina ambaye aliwahi kuinoa Yanga kabla ya kuondoka wakati msimu wa 2017/18 ukielekea ukingoni, alisema, anamkubali beki huyo kuwa ni miongoni mwa walinzi bora ambao amewahi kuwafundisha.

“Niliwahi kuwa Kocha wa Yanga, kwa hiyo Kelvin Yondani namfahamu vizuri kuwa ni beki mzuri, hilo halina ubishi, ni moja ya beki bora ambaye nimewahi kumfundisha. Ni mzoefu na anajua kucheza na washambuliaji tofautitofauti.

“Ingawa ni beki mzuri, lakini haina maana kwamba hawezi kupitika, kwa sababu hata timu bora duniani kuna muda inatokea zinafungwa, kwa hiyo hata yeye pia anaweza akapitwa na washambuliaji wangu,” alisema Lwandamina.

SOMA NA HII  NYOTA WA KMC ATAJA SABABU ZA MEDDIE KAGERE KUFUNGA MABAO