Home Uncategorized MATOLA MAMBO SAFI AZAM FC JINA LAKE LAPENYA JUMLAJUMLA

MATOLA MAMBO SAFI AZAM FC JINA LAKE LAPENYA JUMLAJUMLA


JINA la Kocha Msaidizi wa Simba, Selemani Matola, limepitishwa na viongozi wa Bodi ya Azam FC anayetarajiwa kuwa msaidizi wa Mromania, Aristica Cioba, huku Kocha Mkuu wa Kagera Sugar, Mecky Maxime akichomolewa.

Azam imepanga kuliongezea nguvu benchi lake la ufundi katika kuelekea msimu ujao ambao wamepanga kufanya vema na kikubwa kuchukua ubingwa wa Ligi Kuu Bara uliochukuliwa na Simba kwa misimu mitatu mfululizo.
Matola alijiunga na Simba msimu huu akitokea Polisi Tanzania ambapo kwa sasa ni msaidizi wa Mbelgiji, Sven Vandenbroeck.

Makocha hao wamefanikiwa kubeba ubingwa wa Ligi Kuu Bara na kutinga fainali ya Kombe la Shirikisho la Azam.
Kwa mujibu wa taarifa ambazo imezipata Spoti Xtra, Matola amepitishwa na Bodi ya Azam baada ya kumzidi kwa kura Maxime.

Mtoa taarifa huyo alisema kuwa kabla ya Matola kupitishwa, bodi hiyo ilichagua majina ya makocha bora wawili wazawa wanaofanya vema kwenye ligi, ndiyo akapendekezwa yeye na Maxime, lakini mwisho wa siku Matola akapitishwa baada ya kupata kura nyingi za wajumbe.
Aliongeza kuwa, timu hiyo imepanga kumchukua mzawa kutokana na kulijua vema soka la hapa nchini na miundombinu ya viwanja, hivyo kwa kusaidiana na kocha Mzungu, basi wanaamini watafanya vizuri msimu ujao.

 Kwa sasa msaidizi wa Cioaba ni Mrundi, Bahati Vivier raia wa Burundi.
“Azam imedhamiria kufanya vizuri msimu ujao, hivyo tayari wameanza kuweka mikakati ikiwemo kulisuka benchi la ufundi mapema.

“Hivyo wameanza kwa kumleta kocha mzawa bora mwenye uzoefu na uwezo mkubwa wa kufundisha atakayeweza kumpa ushauri kocha mkuu katika benchi.
“Kati ya makocha hao wawili wazawa, majina yaliyokuwepo ni Maxime na Matola. Jina la Matola ndilo wajumbe wa bodi wamelipitisha, hivyo hadi sasa upo uwezekano mkubwa wa yeye kwenda Azam msimu ujao,” alisema mtoa taarifa huyo. Alipotafutwa Matola kuzungumzia hilo, hakuweza kupatikana.

SOMA NA HII  GWAMBINA HUKU JUU KUNA ISHU YA KUSHUKA PIA, MIPANGO MUHIMU