Home Uncategorized SIMBA YATAJA IDADI YA MAJEMBE ITAKAYOSAJILI MSIMU HUU

SIMBA YATAJA IDADI YA MAJEMBE ITAKAYOSAJILI MSIMU HUU


UONGOZI wa Simba umesema kuwa hesabu kubwa kwa sasa ndani ya Klabu hiyo ni kuongeza majembe matano ya kazi pale dirisha la usajili litakapofunguliwa.

Kwa sasa Simba ni mabingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara ambalo wamelitwaa kwa mara ya tatu mfululizo na kufanya wafikishe jumla ya mataji 21 kibindoni.

Ilifanikiwa kutwaa taji hilo ikiwa na mechi sita mkononi na kwa sasa imeshacheza jumla ya mechi 35 na imebakiwa na mechi tatu ili kukamilisha mzunguko wa pili.

Ofisa Habari wa Simba, Haji Manara amesema kuwa hawana mpango wa kufumua kikosi kizima kwa sasa kwa kuwa kipo imara hivyo wataongeza wachezaji wachache ambao wataongeza nguvu ndani ya kikosi.

“Kwa namna kikosi kilivyo kwa sasa hatuhitaji wachezaji wengi wapya badala yake wachache sana kati ya wanne ama watano hivi hao wataingia kwenye kikosi kuboresha zaidi yale makosa madogomadogo.

“Tunataka kuwa na kikosi imara ambacho kila mchezaji anafanya yake kwa uhuru na uwezo mkubwa kwani hakuna ambaye hana uwezo ndani ya Simba hivyo tunafanya kazi ndogo ya maboresho ili kikosi kiwe na ushindani zaidi.

“Ninajua mashabiki wanapenda kuona tunafanya vurugu kwenye usajili hilo sisi hatuna tunakwenda na mipango na malengo yetu ni kuzidi kuwa imara zaidi na zaidi,” amesema.

Simba ipo nafasi ya kwanza kwenye msimamo ikiwa na pointi 81 baada ya kucheza mechi 35 za ligi.

SOMA NA HII  LUSAJO AJIPA MUDA WA WIKI MOJA KABLA YA KUANZA KUJINOA