Home Uncategorized MUHIMU KUWA MAKINI SASA KATIKA WAKATI HUU WA USAJILI

MUHIMU KUWA MAKINI SASA KATIKA WAKATI HUU WA USAJILI

TAYARI dirisha la usajili limefunguliwa na kila timu ipo sokoni kupambana kupata wale ambao inawahitaji ndani ya timu zao.

 

Timu zote usajili wa Ligi Kuu Bara, Daraja la Kwanza na Ligi ya wanawake ni muhimu wote kufanya usajili na kufanya usajili makini kwa ajili ya timu.

 

Usajili umefunguliwa Agosti Mosi huku ukitarajia kufungwa Agosti 31, usajili wa msimu huu umekuwa mfupi ukilinganisha na ilivyokuwa huko nyuma ambapo usajili huwa unafanywa kwa miezi mitatu kutokana na ligi kuisha mwezi wa tano, lakini kwa sasa hali imekuwa tofauti kutokana na janga la Ugonjwa wa Corona ambao uliikumba dunia hivyo kusababisha masuala ya kimichezo kusimama kwa muda.

 

Kipindi hiki ni kipindi muhimu sana kwa timu zote za ligi kuu, Daraja la Kwanza na wanawake kuhakikisha zinafanya usajili makini kwa ajili ya kuziba nafasi ambazo waliona wazi zilikuwa na mushkeri msimu ulioisha.

Kuna baadhi ya timu tuliziona zilishindwa kufanya vizuri kwenye ligi na kujikuta zikiangukia pua kwa kutofikisha malengo yao hii yote ilikuwa ni kutokana na kutokuwa na vikosi imara ambavyo mwisho wa siku viliwaangusha kwa kufanya vibaya.

 

Mfano mzuri timu kongwe ya Yanga, imeshindwa kutimiza malengo yake ambayo ilijiwekea msimu huu kuhakikisha wanafanikiwa kupata nafasi ya ushiriki wa mashindano ya kimataifa mwakani kwa maana ya Ligi ya Mabingwa Afrika ama  Kombe la Shirikisho kutokana na kutokuwa na kikosi kizuri licha ya usajili wa wachezaji wa kimataifa walioufanya.

 

Hivyo ni wakati wa kila timu kuweza kuangalia mapungufu yake ili mwisho wa siku kuweza kufanya usajili makini na sahihi ambao utaweza kuisaidia timu husika msimu ujao kwa kuleta ushindani katika ligi na si kusajili kwa jili ya mihemko ya watu fulani fulani.

Ni vyema kwa kila klabu ikasajili wachezaji kulingana na matakwa ya timu na si kufanya mashindano yasiyo na misingi alafu mwisho wa siku wachezaji ambao walisajiliwa bila ya uhitaji wanakuja kuzighalimu timu kwenye ligi.

SOMA NA HII  MGOMBEA SIMBA APEWA MILIONI

 

Wasajiliwe wachezaji watakaotoa ushindani na ni vyema wachezaji wote watakaosajiliwa katika timu husika haswa wale wa nje wawe wamefuatiliwa kwa kina mienendo yao na ubora wao ili mwisho wa siku wasisajiliwe wachezaji mizigo ambao watakuja kuleta changamoto katika timu jambo ambalo si sahihi.

 

Kuna baadhi ya timu katika msimu uliomalizika zimejikuta zikishuka daraja kutokana na kushindwa kuonyesha makali kutokana na kutokuwa na wachezaji wenye viwango.

 

Muda ni mfupi mno katika kipindi hiki hivyo ni vyema kila timu ikasajili kwa makini na kuzingatia wakati kwa kupata wachezaji sahihi na si bora wachezaji kwani ligi bora ni ile yenye wachezaji wenye ushindani.