Home Uncategorized NAMNA YANGA ILIVYOSEPA NA POINTI TATU UWANJA WA MKAPA

NAMNA YANGA ILIVYOSEPA NA POINTI TATU UWANJA WA MKAPA


KIKOSI cha Yanga jana, Septemba 13 kimeibuka na ushindi wa bao 1-0 mbele ya Mbeya City kwenye mchezo uliochezwa Uwanja wa Mkapa.

Yanga ilishusha muziki wote wa kazi ndani ya uwanja ambapo dakika 45 licha ya jitihada za Yanga kusaka ushindi ziligonga mwamba baada ya timu zote kwenda mapumziko zikiwa zimetoshana nguvu ya bila kufungana.

Kipindi cha pili Yanga ilifanya mabadiliko kwa kumtoa kiungo Feisal Salum na nafasi yake ikachukuliwa na  Carlos Carlinhos ambaye ni ingizo jipya na alileta mabadiliko kwa upande wa Yanga na alipiga kona mbili hazikuzaa matunda na ile ya tatu aliyopiga dakika ya 86 ilikutana na kichwa cha Lamine Moro.

Ushindi huo unaifanya Yanga kufikisha jumla ya pointi nne ndani ya ligi ikiwa sawa na watani zao wa jadi Simba wakiwa tofauti kwa mabao ya kufunga na kufungana ambapo Simba imefunga mabao matano na Yanga imefunga mabao mawili.

Mbeya City inabidi wajilaumu wenyewe kwa kuwa walipambana dakika 85 kwa kulinda lango lao na kushindwa kufunga ambapo mshambuliaji wao Siraj Juma akiwa kinara wa kufanya majaribio ikiwa ni pamoja na ile ya dakika 66 iliyokwenda nje kidogo ya lango,dakika ya 71 na dakika ya 78 alipaisha.

Kwa upande wa Yanga licha ya kushinda bao 1-0 bado walikosa kufunga mabao kutokana na mikono ya mlinda mlango wa Mbeya City, Haruna Mandanda kutimiza majukumu yake.

Aliokoa hatari ya Mustapha Yassin dakika ya 21 ambaye alikuwa akimwaga maji kutoka pembeni kuelekea lango la Mbeya City ambao wameongezewa uchungu kwa kufungwa bao 1-0 baada ya kutoka kupoteza kwa kufungwa mabao 4-0 mbele ya KMC

Michael Sarpong ambaye alikuwa na uchu wa kutaka kufunga alikwama kumtungua Mandanda huku Feisal Salum naye kiungo wa Yanga alifanya majaribio mawili ambayo yalikwenda nje ya lango ikiwa ni dakika ya 19 na 55.

Mchezo wa Yanga unaofuata ni dhidi ya Kagera Sugar utakaopigwa Uwanja wa Kaitaba,Septemba 19.

SOMA NA HII  SAMATTA AANZA KUFANYA YAKE UTURUKI