Home Uncategorized KAZE WA YANGA AACHWE AFANYE KAZI KWA SASA

KAZE WA YANGA AACHWE AFANYE KAZI KWA SASA

 


KLABU ya Yanga kwa sasa ipo chini ya kocha mpya, Cedric Kaze ambaye tayari amesimamia mechi mbili za ligi na kushinda zote dhidi ya Polisi Tanzania (1-0) na KMC (1-2).

 Yanga kwa sasa katika msimamo kwa ipo nafasi ya pili ikiwa na alama 19 tu baada ya mechi saba na hawajapoteza mchezo wowote mpaka sasa.

 Na huu ndiyo mwanzo wa Kaze ndani ya Yanga ingawa bado safari yake ni ndefu ndani ya kikosi hicho ila endapo tu atapewa nafasi ya kuendelea kufanya kazi ndani ya klabu hiyo.

 

 Kabla ya Kaze kutua Yanga tayari wameondoka makocha wawili na wote ni wa kizungu Luc Eymael  na Zlatico Krmpotic ambao walionekana kushindwa kuimudu timu hiyo na kufungashiwa virago.

 Kaze ndiyo kwanza ameanza na timu ni siku kadhaa hata mwezi hajafikisha na ndiyo kwanza anajaribu kukisuka kikosi chake lakini zile chokochoko za hapa na pale wakati mwingine zinatakiwa ziwekwe kando na yule aliyepewa majukumu aonyeshe kweli kuna kitu ndani yake na  kama inavyojulikana kuwa soka ni mchezo wa wazi ambao unaonekana hadharani.

 Kocha  huyo apewe nafasi ilikuhakikisha kila kitu kinakwenda sawa hakuna asiyefahamu kuwa msimu huu, Yanga inawachezaji bora na hilo liko wazi kilichobaki ni namna ya makocha kuwatumia wachezaji wake tu.

Mashabiki na wapenzi wa soka hususani Yanga kwa muda mrefu walikuwa wakilalamika kuwa wanawachezaji wazuri, lakini timu ilikuwa ikifanya vibaya jambo ambalo lilionekana kuwa ni kero ndiyo maana hata klabu iliamua kuchukua maamuzi magumu kwa kumuondoa kocha ambaye alitangulia.

 

Yanga kwa msimu huu haiihitaji visingizio hasa pale inapopata matokeo mabaya  kama usajili walifanya tena mkubwa tofauti na misimu miwili ya nyuma ambapo walishindwa kufanya hivyo kutokana na kukosa wadhamini.

 Kwa sasa Kampuni ya GSM inafanya kazi kubwa ndani ya Yanga kwa kuidhamini klabu hiyo kwa kuhakikisha kila kitu kinakwenda sawa hivyo hakuna cha kuikwamisha timu hiyo msimu huu wakiamua ni wao wenyewe tu watakuwa wametaka.

SOMA NA HII  TSHISHIMBI: NINAJIFUA KULINDA KIPAJI CHANGU, MUHIMU KUCHUKUA TAHADHARI

 Hivyo ni vizuri kwa sasa wachezaji wakaweka bidii kwa kuhakikisha wanafanya vizuri na kufikia malengo waliojiwekea  kama  klabu.

 Wachezaji wanatakiwa kupambana mpaka hatua ya mwisho kwa kuwa bora na kuonyesha thamani ambayo GSM ambao ni wathamini wao wamewapatia.

 Pia mashabiki kwa kipindi hiki wanatakiwa kutulia na sio kila mmoja kujipa cheo cha ukocha  hiyo kazi ya ukocha  kwa Yanga sasa hivi ni ya Kaze pamoja na Juma Mwambusi wengine mnatakiwa kuwa watazamaji tu na kuwaacha wahusika kufanya kazi yao wenyewe.

 Hivyo ni vizuri Wanayanga  mpeni sapoti  Kaze ili aweze kufanya kazi yake kwa ufanisi mkubwa  ndani ya timu najua  kila  shabiki wa timu hii ndoto yao ni kuona Yanga inafanikiwa kutwaa ubingwa.