Home Uncategorized POLISI TANZANIA:TUTAFUNGA MABAO MENGI KWA MIPIRA ILIYOKUFA

POLISI TANZANIA:TUTAFUNGA MABAO MENGI KWA MIPIRA ILIYOKUFA

 


GEORGE Mketwa, Kocha Msaidizi wa timu ya Polisi Tanzania amesema kuwa mpango mkakati namba moja ndani ya timu hiyo ni kufunga mabao mengi kwa mipira iliyokufa ambayo wamekuwa wakiipata kwenye mechi zao ndani ya ligi.

Kwa sasa Polisi Tanzania ipo nafasi ya saba kwenye msimamo ikiwa na pointi 10 baada ya kucheza mechi tano na imefunga mabao sita. Kinara wa utupiaji ni Marcel Kaheza ambaye amefunga mabao mawili na moja ya bao amefunga kwa mpira wa adhabu.

Mchezo wao unaofuata ni Oktoba 19 itacheza dhidi ya Gwambina FC Uwanja wa Sheikh Amri Abeid na ikimalizana nao itakutana na Yanga, Oktoba 22 Uwanja wa Mkapa saa 1:00 usiku.

Akizungumza na Saleh Jembe, Mketwa amesema kuwa  ushindani ndani ya ligi umewafanya wawe makini katika kutumia nafasi zote ambazo wanazipata ili kushinda mapema jambo litakalowafikisha kwenye mafanikio.

“Kumekuwa na shida kubwa kwenye kutengeneza na kupata nafasi za kufunga, kutokana na jambo hilo tumeamua kubadili mbinu ya ushindi na kutaka kutumia zaidi mipira ile ya kutengwa kufunga mabao mengi.

“Vijana wetu tunawafundisha hilo na tunaona wameanza kuelewa ndio maana mabao yetu mengi ukitufuatilia tunafunga kupitia mipira ya adhabu na tunapata pointi tatu,” amesema.

Mchezo wao uliopita ilishinda bao 1-0 dhidi ya KMC Uwanja wa Uhuru inakutana na Gwambina ambayo imetoka kushinda mabao 2-0 dhidi ya Mtibwa Sugar FC.

 

SOMA NA HII  KIKOSI CHA AZAM FC KITAKACHOANZA LEO DHIDI YA RUVU SHOOTING