Home Uncategorized MAPILATO WA YANGA V SIMBA ACHA KABISA, KADI NYEKUNDU, PENALTI, ZIPO

MAPILATO WA YANGA V SIMBA ACHA KABISA, KADI NYEKUNDU, PENALTI, ZIPO


 UNAAMBIWA waamuzi wa leo wa mchezo wa Yanga na Simba utakaopigwa Uwanja wa Mkapa, kwao kutoa penalti na kadi nyekundu sio ishu ikiwa mchezaji atazingua hivyo leo wachezaji wana kazi kubwa ya kufanya ili kuzipa ushindi timu zao.

Waamuzi ambao wapo kwenye orodha iliyotolewa na Shirikisho la Soka Tanzania ambao ni Ellyi Sasii, Mohamed Mkono, Frank Komba ,Abubakari Mturo, Abdalah Mwinyimkuu na Ramadhan Kayoko hawa ndio mapilato wa leo, cheki rekodi zao zilivyo za moto:-.

Ramadhan Kayoko alikuwa ni mwamuzi wa kati kwenye mechi ya Ngao ya Jamii iliyowakutanisha Simba na Namungo, Agosti 30, Uwanja wa Sheikh Amri Abeid alitoa penalti moja kwa Simba baada ya nyota Bernard Morrison kuchezewa faulo ndani ya 18 na ilifungwa na John Bocco.

Kwenye mchezo huo alitoa jumla ya kadi mbili za njano ambapo moja alimuonyesha Kocha Mkuu wa Simba,Sven Vandenbroeck na moja mchezaji wa Namungo Steve Duah ambaye alicheza faulo kwa Morrison.

Pia kwenye mchezo huo waamuzi wengine aliofanya nao kazi alikuwa ni Frank Komba na Abdallah Mwinyimkuu ambao wote wapo kwenye orodha ya waamuzi wa leo.

Wakati Yanga ikishinda mabao 2-1 dhidi ya KMC Uwanja wa Kirumba, Kayoko alikuwa ni mwamuzi wa kati, alitoa penalti moja kwa Yanga iliyofungwa na Tuisila Kisinda na alimuonyesha kadi ya njano Hassan Kabunda wa KMC na Lamine Moro wa Yanga.Alipewa onyo na bodi ya ligi kutokana na maamuzi hayo.

Kayoko pia kwenye mchezo wa Ligi Kuu Bara aliokuwa mwamuzi wa kati ilikuwa ni Septemba 6 Uwanja wa Majaliwa wakati Namungo ikishinda bao 1-0 dhidi ya Coastal Union alitoa kadi moja ya njano ilikuwa kwa beki wa Namungo, Haruna Shamte.

Septemba 13, Kayoko alipewa jukumu la kuwa mtathimini wa mechi kati ya Yanga 1-0 Mbeya City, alishuhudia kadi moja ya njano kwa Yassin Mustapha wa Yanga.

Waamuzi hawa waliwahi kufanya kazi pamoja pia kwenye dabi ya Kariakoo ilikuwa Julai 12 wakati Simba ikishinda mabao 4-1 ambapo mwamuzi wa kati alikuwa ni Kayoko aliyeibuka kuwa mwamuzi bora kwa msimu wa 2019/20 alishirikiana na Mwinyimkuu pamoja na Frank Komba ambao wote watakuwa na kazi ya kusimamia sheria 17 leo Uwanja wa Mkapa.

SOMA NA HII  VITA YA MZUNGU NA MZAWA LEO UHURU NI BALAA

Kwa upande wa Abdalah Mwinyimkuu yeye alikuwa mwamuzi wa kati kwenye mchezo kati ya Simba 0-1 Ruvu Shooting, Uwanja wa Uhuru ambapo alionyesha kadi nyekundu kwa nyota wa Ruvu Shooting.Shaban Msala na kwenye mchezo huu ilitokea vurugu kwa wachezaji kupigana ngumi njenje ikiwa ni pamoja na Bernard Morrison wa Simba na Juma Nyosso wa Ruvu Shooting, wachezaji hawa wawili walipewa adhabu ya kufungiwa mechi tatu na faini ya laki tano kwa kila mmoja.

Pia aliwapa penalti Simba baada ya Luis Miquissone kuchezewa faulo ndani ya 18, John Bocco aligongesha mwamba penalti hiyo.

Septemba 22,Mwinyimkuu alikuwa mwamuzi wa kati kwenye mchezo kati ya Yanga 1-0 Polisi Tanzania, Uwanja wa Uhuru alionekana kuweza kuumudu mchezo huo uliokuwa na presha. Philip Alando ni kamishna wa mchezo na Pascal Chiganga ni mtadhimini wa waamuzi