Home Namungo FC USHINDI MBELE YA KAGERA SUGAR YAWAONGEZEA HALI YA KUJIAMINI KIMATAIFA NAMUNGO

USHINDI MBELE YA KAGERA SUGAR YAWAONGEZEA HALI YA KUJIAMINI KIMATAIFA NAMUNGO


 HEMED Morroco, Kocha Mkuu wa kikosi cha Namungo FC amesema kuwa ushindi ambao wameupata jana kwenye mchezo wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Kagera Sugar umewaongezea hali ya kujiamini kuelekea kwenye mechi zao za kimataifa .

Machi, 6, Uwanja wa Kaitaba ubao ulisoma Kagera Sugar 0-1 Namungo baada ya dakika 90 kukamilika kwenye mchezo huo wa mzunguko wa pili.

Bao la ushindi kwa Namungo lilipachikwa dakika ya 67 na Sixtus Sabilo kwa shuti kali akiwa ndani ya 18 lililomshinda mlinda mlango wa Kagera Sugar.

Morroco amesema:”Ilikuwa ni kazi kubwa ndani ya uwanja ila mwisho wa siku tumeweza kupata ushindi hiyo ni furaha kwetu kwa kuwa imetuongezea hali ya kujiamini kuelekea kwenye mechi zetu za kimataifa.

“Ukweli ni kwamba tulikuwa tunahitaji pointi tatu nasi tumepata hivyo pongezi kwa wachezaji pamoja na sapoti kutoka kwa mashabiki ambao wamekuwa nasi bega kwa bega,” amesema.

Ushindi huo unaifanya Namungo iwe nafasi ya 9 na pointi zake kibindoni ni 27 baada ya kucheza mechi 18 huku Kagera Sugar ikiwa nafasi ya 13 na pointi zake ni 24 baada ya kucheza mechi 23.

Leo kikosi kinatarajiwa kuondoka kuwafuata Waarabu kwa ajili ya mchezo wa Kombe la Shirikisho.

SOMA NA HII  UWANJA WA MAJALIWA SASA RASMI KWA MATUMIZI....NAMUNGO FC MENO NNJE...LUSAJO ATIA NENO...