Home Burudani ALLY KAMWE: NAFIKIRI RAYVANNY HAJUI KWA NINI ANAGOMBANA NA KONDE BOY

ALLY KAMWE: NAFIKIRI RAYVANNY HAJUI KWA NINI ANAGOMBANA NA KONDE BOY


 RAYVANNY hajui kwa nini anagombana na Harmonize. Na bahati mbaya wanaojua sababu wamegoma kumwambia. Wako kimya.


Ni kama ametupiwa jezi kucheza mchezo asioujua. Rayvanny sio mtu wa matukio. Ni miongoni mwa wanafunzi wa Diamond Platinumz waliohitimu somo la kuwa mwanamuziki mzuri.

 

Ana sauti nzuri, anatunga mashairi makali na ‘melody’ zake zinasikilizika na kuchezeka. Somo pekee ambalo Rayvanny alifeli kulichukua kutoka kwa Diamond ni jinsi gani ya kuishi ‘maisha ya kisanii’. Hili ndilo linalomtesa hivi sasa.Harmonize alichukua vyote kutoka kwa Diamond.

 

Utunzi, juhudi, mipango na mikakati ya kimuziki. Na kizuri zaidi, Harmonize ana ‘Master ya kuishi kisanii’. Alianza kuwa Konde Boy.

Katikati ya safari akajiita Jeshi, na sasa hivi anaitwa Tembo. Ni rahisi sana kumuelewa Harmonize kama uliielewa safari ya kimuziki ya Diamond Platinumz.

 

Kitu kimoja ambacho Rayvanny amechelewa kukijua, Harmonize hana ugomvi na yeye ila ana ugomvi mkubwa na kazi yake.Kuna ukweli unaishi kwenye moyo wa Harmonize kuhusu Rayvanny, lakini kinywa chake kinasema kitu tofauti kabisa.

 

Ulimi wa Harmonize unasema mshindani wake kwa sasa ni Diamond Platinumz, lakini moyo wake unatambua kuwa, mshindani wake wa kweli ni Rayvanny.


Tangu atoke WCB, muziki wa Harmonize umeshuka kiasi. Ameachwa mbali na Diamond Platinumz. Na kibaya zaidi, yuko chini pia ya Rayvanny.


Wimbo wake wa mwisho kuwa na watazamaji wengi kupitia Mtandao wa YOUTUBE ni Kwangwaru aliomshirikisha Diamond.

 

Na huu aliutoa akiwa kwenye kivuli cha WCB. Akiwa na Konde Gang, nyimbo zake hazifanyi vyema sana kwa maana ya kupata watazamaji. Lakini umejiuliza kwa nini bado Harmonize anaendelea kuwa kwenye mijadala ya watu?


Jibu ni sahisi sana, Harmonize anajua njia za kufanya katika kujiweka kwenye kurasa za mbele za magazeti kwa njia tofauti na muziki wake.


Ni mbinu ileile bosi wake wa zamani, Diamond Platinumz alikuwa akiitumia kuwavuruga kina Barnaba, Belle 9 na Marlow.


Belle 9 angekesha studio na kuandika wimbo mkali sana, halafu kesho Diamond angetoka hadharani akiwa anampa Wema Sepetu zawadi ya gari.

SOMA NA HII  ULE UKAKA NA UDADA WA BABA LEVO NA SHILOLE KESHO UKO TENA HEWANI NDANI YA DStv....MSELELEKO NI ULE ULE AISEE...

 

Angefanya hivyo kwa Barnaba na Marlow, kisha keshokutwa yake angekwenda yeye studio na kutoa ngoma yake kali. Wasanii wengi wakali wamepotea kwenye vita na Dimoand kwa kukosa kwao ujanja wa kuishi kisanii.

 

Hili ndilo somo aliloondoka nalo Harmonize na ndio linalomtesa Rayvanny kwa sasa.Nenda katazame nyimbo za Rayvanny kule Youtube. Zinatazamwa sana.

 

Nenda kaangalie idadi ya watu waliosubscribe akaunti yake ya Youtube, ni wengi zaidi ya Harmonize.Jaribu kufuatilia rekodi za mauzo ya albamu ya Rayvanny yalivyo. Yuko mbali kiasi, Huu ndio ukweli mchungu unaomkera Harmonize kwenye njozi zake.


Asingeweza kupambana na Rayvanny kwenye kuimba au kuandika, njia rahisi kwake ni kutumia mbinu ileile iliyokuwa ikitumiwa na Diamond nyakati zile.

 

Vuruga biashara ya mpinzani wako, badili upepo kisha achia kazi zako. Hapa ndipo mahala Harmonize alipofanikiwa sana mbele ya Rayvanny.

Asingekubali kuona urafiki wake na Rayvanny ukaendelea nje.


Watasalimiana wakikutana, atajibu meseji zake WhatsApp lakini hataacha kazi ya Rayvanny iende bila kutia mkono.Fuatilia matendo ya Harmonize tangu atoke WCB.


Yuko makini kwa kutibua kila wimbo unaotolewa na msanii wa Wasafi.Muda ambao Mbosso alikuwa akiitambulisha albamu yake ndio nyakati ambazo Harmonize alimtambulisha Kajala kama mpenzi wake.

 

Utulivu wa watu kuifuatilia Albamu ya Mbosso ukavurugika, stori ikahamia kwa penzi jipya la Kajala na Harmonize.Ni kazi rahisi lakini ni ngumu sana kudili nayo. Kuna nyakati inakufanya usieleweke kabisa.

Leo jamii inavyomshangaa Harmonize ndivyo vilevile ilivyowahi kumshangaa Diamond wakati akitoka na Jokate aliyekuwa rafiki wa Wema.