Meneja wa mshambuliaji kinara wa Simba, Jean Othor Baleke raia wa Congo DR, Clovis Mashisha amekiri kuwa mchezaji huyo ana mkataba na Klabu ya TP Mazembe hivyo yuko Simba kwa Mkopo.
Mashisha amesema hayo wakati akifanyiwa mahojiano maalum na chombo kimoja cha Habari nchini Tanzania baada ya tetesi kusambaa kuwa Baleke si mchezaji wa Simba badala yake yupo klabuni hapo kwa mkopo na muda wowote Mazembe wanaweza kumchukua mchezaji wao.
“Baleke akiwa na miaka 20 amefanya makubwa TP mazembe na Timu ya Taifa ya Congo, kwa hiyo sio mchezaji wa kawaida. Kule kwetu mashabiki wa Mazembe wanamuita Baleke ‘Samatta’.
“Hii ni kwa sababu wanakumbuka kazi nzuri aliyoifanya Mbwana Samatta pale TP Mazembe kabla ya kutimkia KRC Genk ya Ubelgiji, kwa hiyo alipokwenda pale wakasema basi tumepata Samatta mpya,” amesema Mashisha.