Home Habari za michezo MAMELODI SUNDOWN YAANDIKA HISTORIA BAADA YA KUTWAA UBINGWA AFL KWA KUICHAPA WYDAD

MAMELODI SUNDOWN YAANDIKA HISTORIA BAADA YA KUTWAA UBINGWA AFL KWA KUICHAPA WYDAD

WENYEJI, Mamelodi Sundowns wamefanikiwa kutwaa taji la michuano mipya, African Football League baada ya ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Wydad Athletic Club ya Morocco leo Uwanja wa Loftus Versfeld Jijini Pretoria, Afrika Kusini.

Mabao ya Mamelodi Sundowns yamefungwa na mshambuliaji wa Kimataifa wa Namibia Peter Taanyanda Shalulile dakika ya 45 na ushei na kiungo mzawa, Aubrey Maphosa Modiba dakika ya 53.

Mamelodi Sundowns wanakuwa washindi wa kwanza wa African Football League, michuano inayoandaliwa kwa pamoja na FIFA na CAF kwa ushindi wa jumla wa 3-2, kufuatia kufungwa 2-1 kwenye mchezo wa kwanza Jumapili iliyopita mjini Casablanca nchini Morocco.

Kwa ushindi huo, Mamelodi Sundowns wanapata zawadi ya dola za Kimarekani Milioni 4, wakati Wydad Club Athletic inapata dola Milioni 3.

Timu za Al Ahly ya Misri na Esperance ya Tunisia zilizoishia Nusu Fainali kila moja inapata dola Milioni 1.7, wakati TP Mazembe ya DRC, Enyimba ya Nigeria, Petro Atlético ya Angola na Simba ya Tanzania kila moja imepata dola Milioni 1 kwa kushiriki michuano hiyo ya timu nane.

 

SOMA NA HII  TATIZO LA YANGA KWENYE LIGI YA CAFCL LIPO HAPA