Home Habari za michezo MOROCCO TUMAINI JIPYA TAIFA STARS…APEWE MIKOBA YOTE

MOROCCO TUMAINI JIPYA TAIFA STARS…APEWE MIKOBA YOTE

HABARI ZA MICHEZO-TAIFA STARS

KAIMU kocha wa timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, Hemed Suleiman Morocco, ameleta matumaini mapya kwa mashabiki wa soka nchini Tanzania.

Tangu achukue mikoba ya kuinoa Taifa Stars baada ya aliyekuwa kocha wa timu hiyo, Adel Amrouche wa Algeria kufungiwa na Shirikisho la Soka la Afrika (CAF), Morocco ameonyesha uwezo mkubwa wa kuiongoza timu hiyo licha ya mapungufu kadhaa yaliyoonekana.

Kwa sasa, mjadala umeibuka juu ya kama anapaswa kuaminiwa na kupewa mkataba wa kudumu.

Morocco ameiongoza Taifa Stars katika mechi 10, akipata ushindi mara nne, sare nne, na kupoteza mbili pekee, huku zote zikiwa ni za kirafiki. Katika mashindano muhimu, rekodi ya Morocco inaonyesha matumaini makubwa ya timu hiyo kufanya vizuri zaidi katika siku za usoni.

REKODI ZA KUKAIMU

Tangu apewe jukumu la kuinoa Taifa Stars, Morocco ameweza kuleta matokeo chanya katika mechi mbalimbali, hasa zile za mashindano. Akiwa kocha, Morocco ameweka rekodi ya kushinda mechi mbili za kimashindano mfululizo nje ya nchi, kitu ambacho ni nadra kwa timu ya Taifa Stars.

Katika mechi hizo, Tanzania iliibuka na ushindi wa 1-0 dhidi ya Zambia kwenye uwanja wa Levy Mwanawasa na ushindi wa 2-1 dhidi ya Guinea kwenye uwanja wa Yamoussoukro, Ivory Coast.

Pia ameiongoza timu kupata ushindi wa 3-0 dhidi ya Mongolia kwenye mechi ya kirafiki huko Baku, Azerbaijan, na ushindi wa 1-0 dhidi ya Sudan. Zaidi ya hayo, Taifa Stars imefanikiwa kutoka sare na wapinzani wagumu kama Indonesia (0-0), DR Congo (0-0), Zambia (1-1), na Ethiopia (0-0).

Rekodi hizi zinaashiria kuwa Morocco ameleta utulivu na mbinu mpya kwenye kikosi cha Taifa Stars, na amefanikiwa kupambana na timu zenye ubora wa juu katika viwango vya FIFA.

SOMA NA HII  ALI KAMWE AWAPIGA DONGO SIMBA...USAJILI WA JOSHUA MUTALE