Home Uncategorized ISHU YA NIDHAMU KWA WACHEZAJI INAPASWA IANZIE NDANI YA TIMU KABLA YA...

ISHU YA NIDHAMU KWA WACHEZAJI INAPASWA IANZIE NDANI YA TIMU KABLA YA TFF



MATUKIO  mazuri na mabaya kwenye soka kila siku yanatokea huku yale mazuri yakipewa kipaumbele kikubwa kuzungumziwa na timu ama mashabiki kuonyesha kwamba ni namna gani wanaweza kutamba mtaani kutokana na ubora wa mchezaji waliyenaye kwa kile anachokifanya ndani uwanja.
Naona kwa sasa klabu nyingi hapa Bongo zimekuwa na utamaduni wao mpya wa kusifia kizuri cha mchezaji wao na kuchana kibaya cha mpinzani wao jambo ambalo limegeuka na kuwa utamaduni ambao unazidi kukua.
Kwa namna yoyote ile udambwiudambwi wa mchezaji ambao anaonyesha mchezaji wa timu fulani ni rahisi kuonekana kwenye kurasa za mitandao ya kijamii iliyo rasmi ya timu husika hiyo ipo wazi kwa kuwa amefanya vuzuri basi atapambwa na ataimbiwa nyimbo zote nzuri.
Mchezaji huyohuyo akiboronga ninadhani huwa hayo kwenye klabu zetu huwa hayaonekani wahusika wote hutazama pembeni kinachotokea ni kuwaachia mashabiki wa timu pinzani kuanza kupanza sauti zao wakiwakumbusha wachezaji wa timu pinzani.
Mfano mzuri kwa sasa ni rahisi kuona bao alilofunga Jonas Mkude mbele ya Alliance kwenye ukurasa wa Instagram wa Simba lakini itakuwa ngumu kuona kipande cha huyohuyo Mkude akimpiga kiwiko mchezaji wa Biashara United.
Kwa upande wa watani zao wa jadi Yanga ni rahisi kuona bao alilofunga Bernard Morrison kwenye akaunti zao ila ni ngumu kuona kiwiko cha Morrison alichompiga mchezaji wa Tanzania Prisons.
Hii kwa sasa inabidi itazamwe kwa ukaribu na timu zenyewe ambazo ndio zinawalea wachezaji na zinaingia mkataba na wachezaji endapo kila kizuri anachofanya mchezaji kikizungumzwa basi na pale ambapo anakosea aambiwe itaongeza uthamani na heshima kwa kila atakayepata nafasi ya kuzitumikia timu hizo.
Wachezaji pia wanapaswa waelewe kwamba mpira sio vita bali ni burudani ambayo inatazamwa na wengi nina amini iwapo klabu zitakuwa zikifuatilia masuala ya nidhamu kwa wachezaji na kutoa adhabu pale inapostahili wachezaji wangekuwa wanacheza kwa juhudi isiyo ya kawaida.
Leo hii ikitokea kosa kwa mchezaji la kinidhamu ndani ya Uwanja klabu kubwa zinakuwa kimya zinaskilizia Kamati ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) lifanye maamuzi hii sio sawa.
Kila kitu kikiwa mikononi mwa TFF klabu itafanya nini kwa ajili ya mchezaji? Mchezaji yupi ambaye amefanya makosa na klabu ikampa adhabu ambayo itamfanya awe  mfano kwa wengine.
Nina amini ili kujenga timu bora kuna umuhimu wa kutazama aina ya mfumo ambao timu zetu zinatumia. Klabu kubwa na ndogo ni muhimu kubadilika na kufanya mambo ambayo yatakuwa tija wa wachezaji na mashabiki.
Kamati ya nidhamu inapaswa ianzie ndani ya timu husika na TFF wao wawe wanamalizia masuala yanayotokea ndani ya uwanja itaongeza ufanisi kwa wachezaji na kuongeza ulinzi kwa wachezaji wa timu pinzani.
SOMA NA HII  BREAKING:LWANGA ASAINI DILI JIPYA SIMBA