Home Uncategorized JOKATE AWAITA MASHABIKI WA YANGA TAIFA WAKAIMALIZE SIMBA

JOKATE AWAITA MASHABIKI WA YANGA TAIFA WAKAIMALIZE SIMBA




Na Mwandishi wetu
MMOJA wa wapenzi maarufu wa Yanga,Ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe, Jokate Mwegello, amewataka wenzake wapenzi wa timu hiyo kujitokeza kwa wingi Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam wakati watakapopambana na watani wao wa jadi, Simba.


Katika mchezo huo wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Yanga ndio watakaokuwa wenyeji, wakiwa na mzuka wa kushinda ili kuwatia presha Simba kuelekea mbio za ubingwa wa ligi hiyo.


Ikumbukwe katika mchezo wa mzunguko wa kwanza kwenye uwanja huo, timu zilitoka sare ya mabao 2-2, wenyeji Simba wakiwa wa kwanza kupata mabao mawili, kabla ya Yanga kusawazisha yote, tena ndani ya dakika tatu tu.


Akizungumza na gazeti hili jana Alhamisi, Jokate ambaye ni Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe, Pwani, alisema kuwa Yanga watashinda mchezo huo wa Jumapili kutokana na ubora wa kikosi chao.


“Sina wasiwasi na timu yangu ya Yanga, naamini itashinda tu mbele ya Simba Jumapili, niwaombe mashabiki wa Yanga tujitokeze kwa wingi uwanjani wakiwa wamevaa jezi za timu yetu ili tuwape morali wachezaji wetu waweze kupambana na kupata ushindi,” alisema Jokate aliyeitikisa fani ya urembo mwaka 2006, ikidaiwa ndiye aliyestahili kutwaa taji la Miss Tanzania badala ya aliyepewa ushindi.


Alisema kwa kuwa kauli mbiu ya Yanga kuelekea mchezo huo ni vaa kibingwa, basi kila shabiki avae jezi ya mchezaji wa timu hiyo anayempenda ili kunogesha siku hiyo wakiwa kama wenyeji wa mchezo.


“Kwa sasa nipo kwenye ziara huku vijijini, ila natamani iwepo uwanjani siku hiyo, lakini hata kama nikishindwa kwenda, najua vijana wetu hawataniangusha, tutashinda tu,” alisisitiza.


Kwa upande wake, Meneja Masoko na Mawasiliano wa GSM Group, Matina Nkurlu, alisema wametengeneza jezi za kutosha ili kila shabiki wa Yanga aweze kupata na kwenda nayo uwanjani Jumapili kushuhudia pambano hilo.


“GSM tunafahamu mvuto wa mchezo huo, na tukiwa kama wadhamini wa Yanga na watengenezaji rasmi wa jezi za klabu hiyo, tumehakikisha tunatengeneza jezi za kutosha zenye ubora wa hali ya juu ili kukidhi mahitaji ya Wanayanga.


“Jezi zimeshaanza kuuzwa katika maeneo mbalimbali na zaidi maduka ya GSM yaliyopo Mlimani City, Pugu Mall, Lumumba na kwingineko hivyo kila shabiki wa Yanga ahakikishe ananunua jezi halisi (original) ya Yanga na kuepuka kununua zile za mitaani ambazo hazina maslahi yoyote na klabu yao,” alisema.


Alisema jezi zao hizo zipo katika ubora wa hali ya juu unaolingana na hadhi klabu ya Yanga. Niwaombe wanayanga wasikubali kununua jezi za mitaani ambazo ni za wajanja wachache ambao wamekuwa wakipiga fedha kwa kupitia nembo ya Wanajangwani hao.

SOMA NA HII  NAHODHA STARS: TUNAPENYA LEO MBELE YA KENYA, MASHABIKI MTUPE SAPOTI