Home Uncategorized GUMZO LA UNUNUZI WA NEWASTLE NA KASHFA YA KIFO CHA MWANDISHI KASHOGGI

GUMZO LA UNUNUZI WA NEWASTLE NA KASHFA YA KIFO CHA MWANDISHI KASHOGGI





Na Saleh Ally
WAKATI dunia ikipambana na Corona, gumzo kubwa limeibuka katika Ligi Kuu England baada ya kuonekana mwana wa mfalme wa Saudi Arabia, Mohamed bin Salman yuko katika hatua ya mwisho kuinunua Newcastle United.


Newcastle United ni moja ya timu, yenye nguvu ya kifedha na mashabiki wengi kwa England ingawa haiwezi kuwa kama kina Manchester United, Chelsea, Arsenal Liverpool na Manchester City.

Ujio wa bin Salman unaweza kuwa tamaa ya mashabiki wa Newcastle lakini maswali yaliyoibuka ni utamaduni na usafi wa mwana mfalme huyo.


Vizuri kwanza ungemfahamu kidogo mwana wa Mfalme, Mohamed bin Salman ambaye kupitia kampuni yake ya Saudi Arabia Public Investment Fund amekubali kutoa kitita cha pauni miliini 300 kuinunua Newcastle.


Mmiliki wake wa sasa Mike Ashley ambaye amekuwa nayo kwa miaka 13 sasa ikiwa Premier League na wakati mwingine Premiership tayari amekubali kuchukua mpunga wa mwana mfalme huyo ambaye kama kila kitu kikikamilika, anachukua rekodi ya kuwa mmiliki tajiri zaidi wa klabu ya Premier League.


Yeye anatokea katika familia ya kifalme, mamilioni ambayo utajiri wake kwa jumla ni pauni trilioni 1.3. Lakini yeye mwana wa mfalme, utajiri wake pekee ni zaidi ya pauni bilioni 7 nje ya kampuni yake pia familia ya kifalme, hivyo kwanza pauni milioni 300, kwake si kitu cha kumshitua.


Kampuni yake ambayo ataitumia kununua Newcastle na makampuni yake baadhi utajiri wake ni pauni bilioni 260.


Matajiri ambao angalau wanaweza kumsogelea kwa karibu bin Salman ambao wanamiliki klabu za Ligi Kuu England ni Sheikh Mansour wa Manchester City (pauni 23.3B), Roman Abramovic wa Chelsea (pauni 9.6B), Stan Kroenke wa Arsenal (pauni 6.8b) na Guo Guangehang wa Wolves mwenye pauni bilioni 52.


Gumzo kama nilivyokueleza awali ni usafi wa mikono yake na utamaduni wa nchi anayotokea na England ambako Saudi Arabia kutokana na kushika misingi ya dini ya Kiislamu, hawawezi kukubali masuala ya ushoga wakati England hayo ni maisha ya kawaida.

Hili la utamaduni limezua maswali mengi na juzi kipindi cha TalkSport katika mtandao huo kilipata watu wengi sana na inaonekana asilimia 35, wangependa bin Salman ainunue Newcastle na wengine wakipinga kupitia utamaduni pamoja na kuamini bin Salman yuko katika kashfa inayomtafuna na huenda imechangia kwa kiasi kikubwa kuongeza nguvu ya kutaka kuinunua Newcastle.


Hii ni ile kashfa ya kifo cha mwandishi maarufu wa habari wa Washington Post, Jamal KAshoggi ambaye aliuawa kikatili kwenye ubalozi wa Saudi Arabia nchini Uturuki.


Bin Salman amekuwa akikanusha mara kwa mara mauaji hayo ya Kashoggi lakini inaonekana kukanusha kwake bado hakujaeleweka vizuri na wadau wengi wanaolijadili suala la yeye kuinunua Newcastle wanaona kama anataka kuutumia mpira wa England kutokana na ukubwa wake kujisafisha.


Wale wanaofurahia wanaamini Newcastle itabadilika, kumbukumbu ikiwa hivi kuwa kabla ya kuingia kwa mabilionea wa Chelsea na Manchester City, Klabu ya Newcastle ilikuwa kubwa na maarufu zaidi ya klabu hizo mbili.


Lakini baada ya Abramovic kuingia na kuanza na usajili wa Andriy Shevchenko, Michael Ballack na nyota wengine huku Man City ikimsajili Robinho kutoka Real Madrid, mambo yakabadilika.


Matumaini ya mashabiki wa Newcastle wasioangalia utamaduni wa kashfa za bin Salman, wanaamini nyota mbalimbali kama Kylian Mbappe na wengine watasajiliwa na Newcastle United na kuanzia hapo, maisha mapya ya klabu hiyo yataanza na itakuwa ni zile zinazosubiriwa kushiriki Ligi ya Mabingwa Ulaya huku zikiwania ubingwa wa England na si kusubiri kubahatisha kucheza Europa League.
SOMA NA HII  AZAM FC BADO WANAUHITAJI UBINGWA