Home Uncategorized CIOABA WA AZAM FC KUIVAA MBEYA CITY BILA NYOTA WAKE MMOJA

CIOABA WA AZAM FC KUIVAA MBEYA CITY BILA NYOTA WAKE MMOJA


 ARISTICA Cioaba, Kocha Mkuu wa Azam FC atakiongoza kikosi chake kesho kumenyana na Mbeya City Uwanja wa Sokoine bila nyota wake mmoja, Agrey Morris.

Nyota huyo ameachwa Dar na kikosi ambacho kilisafiri jana, Septemba 18 kuifuata Mbeya kwa ajili ya mchezo wa Ligi Kuu Bara unaotarajiwa kuwa na ushindani mkubwa. 

Ofisa Habari wa Azam FC, Zakaria Thabit amesema kuwa msafara wao wa wachezaji umeambatana wachezaji 24 huku Morris akibaki Dar kwa ajili ya kuendelea na matibabu.


“Mchezaji mmoja amebaki Dar ambaye ni Morris yeye alipata majeraha kwenye mchezo wetu dhidi ya Coastal Union lakini maendeleo yake ni mazuri.

“Kikubwa ambacho tunakihitaji kwa sasa ni kuona timu inaendelea kupata matokeo ndani ya mechi zake zote hivyo katika hilo tunaomba mashabiki waendelee kutupa sapoti,” amesema.


Azam FC inakutana na Mbeya City ambayo imetoka kupoteza kwa kufungwa bao 1-0 mbele ya Yanga mchezo uliochezwa Uwanja wa Mkapa, Azam FC mchezo wake wa mwisho ilishinda mabao 2-0 mbele ya Coastal Union.

Unakuwa ni mchezo wa kwanza kwa Azam FC kucheza nje ya Dar  kwa msimu wa 2020/21 huku Mbeya City nao ukiwa ni mchezo wao wa kwanza kucheza nyumbani kwa kuwa mechi zake zote mbili ilicheza Dar ikiwa ugenini.


Ilianza kufungua pazia la ligi kwa kucheza na KMC Uwanja wa Uhuru na ilipoteza kwa kufungwa mabao 4-0 kabla ya kumaliza hesabu za raundi ya pili kwa kufungwa bao 1-0 mbele ya Yanga hivyo kesho Mbeya City itawakaribisha Azam FC.

SOMA NA HII  SABABU ZA MKUDE KUCHIMBISHWA SIMBA ZATAJWA