Home Uncategorized SIMBA YAANZA KUIPIGIA HESABU BIASHARA UNITED

SIMBA YAANZA KUIPIGIA HESABU BIASHARA UNITED

 


UONGOZI wa Simba umesema kuwa upo tayari kwa ajili ya mchezo wao wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Biashara United utakaopigwa Septemba 20, Uwanja wa Mkapa.


Mchezo huo utakuwa ni wa kwanza kwa Simba kucheza ndani ya Dar es Salaam kwa msimu wa 2020/21 ikiwa chini ya Kocha Mkuu, Sven Vandenbroeck. 


Simba wakiwa na kibarua cha kutetea taji la Ligi Kuu Bara tayari imeshayeyusha pointi mbili mazima kati ya sita ilizokuwa ikizisaka ambapo ilianza kwa kumenyana na Ihefu, Septemba 6 Uwanja wa Sokoine na ilishinda kwa mabao 2-1 kisha Septemba 12 ikalazimisha sare ya kufungana bao 1-1 mbele ya Mtibwa Sugar. 


Ofisa Habari wa Simba, Haji Manara amesema kuwa hakuna namna nyingine ambayo watakwenda kufanya mbele ya Biashara United zaidi ya kurejesha furaha kwa mashabiki wa timu hiyo.


Msimu uliopita Simba ilipokutana na Biashara United,  Uwanja wa Mkapa iliibuka na ushindi wa mabao 3-1 na moja ya tukio la kukumbukwa ni uimara wa mlinda mlango namba moja wa Biashara United,  Daniel Mgore ambaye aliipangua penalti ya mshambuliaji namba moja wa Simba, Meddie Kagere. 


Unatarajiwa kuwa mchezo wenye ushindani kwa kuwa Biashara United haijayeyusha pointi kwenye mechi zake zote mbili mchezo wake wa mzunguko wa pili imetoka kuwatungua Mwadui FC bao 1-0.


Kibindoni Biashara United inayonolewa na Francis Baraza ina pointi sita na mabao mawili inakutana na Simba yenye pointi nne na mabao matatu.

SOMA NA HII  SAID MAKAPU ATAJA SABABU YA KUANZA KIKOSI CHA KWANZA NDANI YA YANGA