Home Uncategorized MASHINE MPYA SIMBA YAPANIA KUFANYA MAKUBWA

MASHINE MPYA SIMBA YAPANIA KUFANYA MAKUBWA


 KIUNGO mkabaji wa kimataifa wa timu ya Taifa ya Uganda, Taddeo Lwanga ambaye ni ingizo jipya ndani ya Klabu ya Simba baada ya kusaini dili la miaka miwili kuitumikia klabu hiyo amesema kuwa atapambana kuipa matokeo chanya timu yake.


Lwanga ndani ya Simba rasmi Desemba 2 alitambulishwa na kupewa jezi namba nne ambayo ilikuwa inavaliwa na mkata umeme Gerson Fraga ambaye kwa sasa anatibu majeraha yake akiwa nchini Brazil.


Nyota huyo ambaye amewahi kuzichezea timu za Express FC, SCV Kampala, Vipers FC na Tanta FC ameweka bayana kwamba hatawaangusha mabosi wake.

“Nimekuja ndani ya Simba ambayo ni timu kubwa na yenye mashabiki wengi, nina amini kwamba nitafanya kile ambacho kinatakiwa ili kuweza kufikia malengo.

“Kikubwa mashabiki watupe sapoti katika michezo yetu na ninaona kwamba kuna nafasi ya kufanya vizuri kitaifa na kimataifa ni suala la wakati tu,” amesema.

Simba imetinga hatua ya mtoano baada ya jana Desemba 5 Uwanja wa Mkapa kulazimisha sare ya bila kufungana na Plateau United ya Nigeria kwa kuwa mchezo wa kwanza ilishinda bao 1-0 ikiwa ugenini.
SOMA NA HII  COASTAL UNION YAZITAKA POINTI TATU ZA NAMUNGO