Home Uncategorized SIMBA YAPIGA HODI CAF KWA SABABU YA MASHABIKI

SIMBA YAPIGA HODI CAF KWA SABABU YA MASHABIKI


OFISA Habari wa Simba, Haji Manara amesema kuwa kuelekea mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya FC Platinum kila kitu kipo sawa kwa upande wa maandalizi huku wakiwa wameomba kupewa kibali cha kuongeza idadi ya mashabiki.

Mara amesema Klabu ya Simba, imeliomba Shirikisho la Soka Afrika (Caf) kuwaongezea idadi ya watu kutoka 50% ya mashabiki kuingia uwanjani katika mechi dhidi ya Platinum ya Zimbabwe inayotarajiwa kuchezwa Januari 6, 2021, Uwanja wa Mkapa.


Katika mechi dhidi ya Plateau, Caf iliwapa Simba nafasi ya kuingiza mashabiki 50% ya uwezo wa Uwanja wa Mkapa kwa hofu ya ugonjwa wa Covid 19.

Manara amesema kuwa wanataka zaidi ya idadi hiyo kutokana na hali ya Tanzania kiusalama wa afya ilivyo jambo ambalo limewafanya watume maombi ya kupewa kibali cha uongezeko la mashabiki zaidi.


Pia ameongeza kuwa kutakuwa na punguzo la viingilio ndani ya uwanja ambapo awali ilipangwa kuwa 7,000 ila sasa itakuwa 5,000 mzunguko VIP B na C ilipangwa iwe 20,000 lakini sasa itakuwa 15,000.

Lakini mashabiki wanatakiwa kupata tiketi kabla ya Jumatatu ikiwa watahitaji kununua siku ya mchezo basi watakuwa na kazi ya kununua tiketi kwa bei ile ya awali.

Kwenye mchezo huo Simba ina kazi ya kusaka ushindi kwa kuwa ilipoteza mchezo wa kwanza nchini Zimbabwe kwa kufungwa bao 1-0.

Inatakiwa kufanya jambo moja pekee, kushinda zaidi ya mabao mawili huku ikilinda lango lake lisitikiswe ndani ya dakika 90.
SOMA NA HII  NYOTA WA YANGA AMALIZANA NA ALLIANCE FC