Home Uncategorized SIMBA YAIPELEKA YANGA MDOMONI MWA AL AHLY

SIMBA YAIPELEKA YANGA MDOMONI MWA AL AHLY


KAMA zali tu vifaa vipya ambavyo vitavaa jezi za Yanga msimu ujao vina nafasi kubwa ya kukipiga dhidi ya timu za TP Mazembe na Al Ahly, hiyo ni baada ya wapinzani wao Simba kuwakutanisha na timu hizo.

Hatua hiyo imekuja baada ya Yanga kupata nafasi ya kushiriki katika Ligi ya Mabingwa Afrika ambapo kwa msimu ujao watacheza huko baada ya kupata nafasi kutoka kwa Shirikisho la Soka Afrika (Caf).

Taarifa rasmi ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) iliyotolewa jana Jumanne imeeleza kuwa Yanga wamepata nafasi hiyo baada ya kuongezwa kwa timu za Tanzania katika michuano ya kimataifa iliyo chini ya Caf kutokana na mafanikio ya Simba msimu uliopita wa 2018/19.

TFF imeeleza kuwa timu mbili zitawakilisha Ligi ya Mabingwa Afrika na mbili nyingine zitashiriki katika Kombe la Shirikisho Afrika.

Nafasi ya kushiriki Kombe la Shirikisho imekwenda kwa Azam FC ambao ni mabingwa wa Kombe la FA na Timu ya Manispaa ya Kinondoni (KMC) ambao wenyewe wamepata nafasi hiyo ya upendeleo kwa kuwa walishika nafasi ya nne katika Ligi Kuu Bara.

Taarifa hiyo imefafanua kuwa kutokana na Simba kufika hatua ya robo fainali msimu uliopita, kumeifanya Tanzania kufikia vigezo vya CAF katika kupanda ubora wa kiwango cha nchi upande wa klabu na kufikia nafasi ya 12 kwenye viwango vya ubora.

Tayari CAF imefungua dirisha kwa mashirikisho kusajili timu kupitia mtandao wa CMS, mwisho wa kufanya hivyo ni Juni 30, mwaka huu. Rais wa TFF, Wallance Karia amezitaka timu zilizopata nafasi kusajili kwa umakini ili kujiandaa na mshindano hayo kulinda nafasi nne kwenye michuano ya CAF.

SOMA NA HII  NYOTA WATATU WA SIMBA KUIKOSA AZAM FC KESHO TAIFA