Home Uncategorized MUANGOLA WA YANGA APEWA JEZI YA SIBOMANA

MUANGOLA WA YANGA APEWA JEZI YA SIBOMANA


 CARLOS Stenio Fernandes Guimaraes do Carmo maarufu kwa jina la Carlinhos, ndani ya Yanga amekabidhiwa jezi namba 11 iliyokuwa ikivaliwa na kiungo mshambuliaji wa timu hiyo, Patrick Sibomana raia wa Rwanda.

 

Sibomana ambaye mkataba wake umesitishwa na Yanga na kupewa mkono wa kwaheri, msimu uliopita alikuwa akiivaa jezi hiyo kabla ya kukabidhiwa Carlinhos.

 

Jana Jumatano wakati Carlinhos alipofika mazoezini kwa mara ya kwanza, alikaribishwa kwa staili ya kucheza muziki na kiungo mkabaji wa timu hiyo, Mkongomani, Mukoko Tonombe.


Tukio hilo la aina yake lilifanyika kwenye Uwanja wa Chuo cha Sheria, Ubungo jijini Dar es Salaam ambako timu hiyo inafanya mazoezi kujiandaa na msimu wa 2020/21.

 

Mshambuliaji huyo alitua nchini juzi Jumanne akitokea nyumbani kwao Angola tayari kwa ajili ya kuichezea timu hiyo aliyojiunga nayo kwa mkataba wa miaka miwili.

 

Yanga ikiwa mazoezini, imekuwa na utamaduni wa kuwapokea wachezaji wapya kwa kuwataka wachomekee jezi na kupigiwa makofi, kisha kucheza muziki huku akiwa amezungukwa na wenzake na mmoja kumkaribisha.

 

 

Carlinhos jana Jumatano ilikuwa siku yake ya kukaribishwa ambapo alipofika mazoezini kwa mara ya kwanza, Tonombe alichukua jukumu la kumkaribisha na kumuelekeza namna ya kucheza muziki huku wenzao wakiwapigia makofi.

SOMA NA HII  SABABU ZA KUPIGWA CHINI KOCHA MKUU WA YANGA NI HIZI HAPA