Home Uncategorized YANGA YAIFUATA KAGERA SUGAR NA MATUMAINI YA KUTOSHA

YANGA YAIFUATA KAGERA SUGAR NA MATUMAINI YA KUTOSHA


 KIKOSI cha Yanga, leo Septemba 17 kimekwea pipa kuelekea Bukoba kwa ajili ya mchezo wao wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Kagera Sugar kikiwa kimebeba matumaini kibao ya kuibuka na ushindi.


Matumaini hayo yanachangiwa na ushindi ambao waliupata jana, Septemba 16 Uwanja wa Azam Complex wa mabao 2-0 mbele ya Mlandege FC kwenye mchezo wa kirafiki.


Mchezo huo ambao ulikuwa na malengo ya kuboresha kikosi hicho ambacho hakijawa na muda mrefu wa kufanya mazoezi kwa pamoja ulikuwa ni wa ushindani mkubwa kwa timu zote mbili.


Mabao ya Yanga yalipachikwa kimiani na nyota wake wapya ambao ni pamoja na Wazir Junior aliyeibukia Yanga akitokea Mbao FC pamoja na Tunombe Mukoko aliyeibukia Yanga akitokea AS Vita ya Congo.

Hersi Said, Mkurugenzi wa Uwekezaji wa Kampuni ya GSM ambao ni wadhamini wa Klabu ya Yanga amesema kuwa wanaamini kwa namna walivyofanya usajili makini timu itakuwa na matokeo mazuri ndani ya uwanja.

“Timu imefanya usajili mzuri na makini, kwa namna kikosi kilivyo imani ni kwamba tutapata matokeo mazuri ambayo yatatufanya tuweze kutwaa mataji jambo ambalo ni furaha kwetu na mashabiki kiujumla,” amesema.

Yanga itamenyana na Kagera Sugar, Septemba 19 Uwanja wa Kaitaba ambapo inashuka uwanjani ikiwa na kumbukumbu ya kushinda bao 1-0 kwenye mchezo wa ligi mbele ya Mbeya City.

Kagera Sugar wao walitoka kulazimisha sare ya bila kufungana mbele ya Gwambina FC. Unakuwa ni mchezo wa pili kwa Kagera Sugar kucheza wakiwa nyumbani ambapo ule wa kwanza walipoteza kwa kufungwa bao 1-0 mbele ya JKT Tanzania.


Kwa upande wa Yanga ni mchezo wa kwanza kucheza nje ya Dar kwa msimu mpya wa 2020/21 ule wa kwanza dhidi ya Tanzania Prisons kwenye sare ya kufungana bao 1-1 pamoja na ule wa ushindi mbele ya Mbeya City yote ilichezwa Uwanja wa Mkapa.

SOMA NA HII  SIMBA YAINGIA ANGA ZA KIPA MRUNDI, ALIWABANIA YANGA