Home Uncategorized KILICHO NYUMA YA USHINDI NI MAANDALIZI, TUNAHITAJI KUONA LIGI BORA

KILICHO NYUMA YA USHINDI NI MAANDALIZI, TUNAHITAJI KUONA LIGI BORA

 


LIGI Kuu Tanzania Bara imeanza kutimua vumbi Septemba 6 na 7 ilikamilisha mzunguko wa kwanza kwa ajili ya mbio za kumsaka bingwa mpya wa msimu wa 2020/21.


Kwa sasa taji lipo mikononi mwa Simba ambao walitwaa msimu uliopita baada ya kucheza mechi 38 na kujikusanyia pointi 88.

 

Simba ilifungua pazia la ligi kwa kumenyana na Ihefu FC ambapo ilishinda mabao 2-1, Uwanja wa Sokoine Mbeya. Yanga ilitoshana nguvu kwa kufungana bao 1-1 na Tanzania Prisons Uwanja wa Mkapa.

 

Kwa upande wa mipango licha ya kwamba muda ulikuwa mfupi katika maandalizi kutokana na janga la Corona bado kila mmoja amejipanga kufanya vizuri.

 

Ninaamini kwamba timu zimejipanga kikamilifu katika msimu huu ambapo tumeshuhudia timu mbalimbali zikifanya sajili zilizo imara na za kushtua baada ya kuleta nyota wakubwa.

 

Hali hii imetokana na ubora wa ligi yetu ambayo inaendelea kukua siku hadi siku kiasi cha kuwavutia nyota mbalimbali tofauti na kipindi cha nyuma ambapo haikuwa rahisi kuona nyota kutoka timu kubwa wanakuja kusajiliwa katika klabu zetu.

 

Hii ni nyota njema katika ligi yetu ambapo lengo lake ni kuona inasonga mbele zaidi ili kupata timu bora ya taifa.

 

Hivyo basi naamini usajili ambao umefanyika na timu mbalimbali za ligi kuu, ni wazi kila shabiki na mdau wa soka angependa kuona kandanda safi uwanjani likionyeshwa na kila timu ili kuleta ushindani wa kweli ambao utasababisha ligi kuwa bora.

 

Kila shabiki kwa sasa anatarajia kuona timu yake ikipambana na kupata pointi tatu kwa uhalali bila makelele ambayo yalikuwa yakitokea msimu uliopita.

 

Kuhusu waamuzi kushindwa kupewa zigo la lawama pale ambapo mchezo unakamilika hatutarajii haya kutokea kwa msimu mpya wa 2020/21.

 

Pia timu kutegemea kubebwa na matokeo ya mezani hilo pia halitakuwepo kwa kuwa usajili uliofanywa ulikuwa ni mapendekezo ya benchi la ufundi waachwe wafanye kazi.

 

Kila timu inahitaji kujiamini bila ya kujali inakutana na timu gani katika mechi itakazocheza na matokeo yake timu zihamasishe wachezaji  wao ili kuleta ushindani na kupata matokeo mazuri.

SOMA NA HII  KAKOLANYA ACHEKELEA MAISHA NDANI YA SIMBA

 

Kila timu imepata muda wa kutosha wa kujiandaa kuelekea msimu mpya, hivyo hatutarajii kusikia malalamiko na badala yake kila timu ijipange.

 

Wadau wanahitaji kuona bingwa ambaye atatoka jasho kwa kupambana na sio kwa kubebwa ndani ya uwanja.

 

Wachezaji kwa ujumla wanatakiwa kutambua majukumu yao kuhakikisha kila mmoja anafanya kile kilichosababisha kusajiliwa katika timu husika.

 

Pia kuna baadhi ya makocha wamekuwa hawaonyeshi viwango katika timu zao na timu zitakapofanya vibaya wanatoa malalamiko kwa waamuzi kutochezesha vyema kwa kufanya ndio mwamvuli wa kujifichia makosa yao.

Katika hilo pia makocha ni lazima mbadilike, jipangeni wadau wanahitaji dakika 90 ndizo zitoe maamuzi.Suala la ushindi ni lazima kuwe na maandalizi mazuri na inawezekana.